Thursday 16 March 2017

Hashim Rungwe amvaa Dkt. Mwakyembe.....Amtaka asiivuruge TLS


Mwenyekiti wa CHAUMMA, Hashim Rungwe amemtaka Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Harrison Mwakyembe kuacha kuingilia mambo yanayohusu chama cha wanasheria Tanganyika (TLS) hasa kwenye suala uchaguzi wa kumsaka Rais wa chama hicho

Akijibu maswali ya wananchi kwenye kipindi cha KIKAANGONI kinachorushwa katika ukurasa wa Facebook EATV, Mh. Rungwe amesema kuwa TLS ina utaratibu wake wa kuendeshwa na kamwe haiwezi kupelekwa kama jinsi waziri anavyotaka kwani chama hicho kinaongozwa kwa sheria na kanuni.

“Yeye kama Waziri maoni yake ni muhimu, lakini  anasema vijana hawa wawili wana maoni ya kisiasa yaani Lissu na mwenzake lakini wakati huo huo yeye ni waziri na mpaka amefika hapo yupo ndani ya chama cha kisiasa. na amevaa kofia mbili. TLS  haiwezi kuendeshwa kama anavyotaka yeye, huwezi kutengeneza utaratibu nje ya utaratibu. Tuheshimu pia taaluma za watu." Rungwe alifunguka.

Aidha Rungwe ambaye pia ni Wakili wa Mahakama Kuu na Mwanachama wa chama hicho ameongeza kuwa katika chama hicho hakuna sheria ambayo inamzuia mwanasiasa yoyote kugombea nafasi na kuongeza kwamba kuwazuia upinzani wakati waliomo kwenye chama tawala wanaruhusiwa ni kutengeneza chuki ndani ya jamii na nchi kwa ujumla

"Kutengeneza chuki kwa makusudi it's a great crime, hasa chuki ikitengenezwa na viongozi waliopo madarakani, ambao wamepewa dhamana ya kuwaongoza wananchi yeye atuache na TLS yetu, kama itaonesha watu hawa hawaruhusiwi kugombea basi watazuiliwa kwasababu watu wanaochuja wagombea ni sisi wenyewe". Amesema

Hivi karibuni Waziri huyo wa Sheria na Katiba alinukuliwa akisema kuwa serikali haiwezi kuona (TLS) ikinajiingiza katika siasa na kuongeza kuwa kama wanataka hivyo, basi serikali haitasita kuifuta Sheria ya TLS Sura ya 307 iliyoanzisha chama hicho cha wanasheria.

No comments:

Post a Comment