Tuesday 14 March 2017

Wivu wa Mapenzi Wasababisha Kifo cha Kichanga


MKAZI wa Kijiji cha Chiwana wilayani humu, Said Kassim (20), ametiwa mbaroni kwa tuhuma za kumuua mtoto katika tukio la ugomvi na mkewe chanzo kikidaiwa ni wivu wa mapenzi.

Kamanda wa Polisi mkoani Ruvuma, Zubery Mwombeji alisema kuwa tukio hilo lilitokea Machi 9, mwaka huu saa 10 jioni.

Kamanda Mwombeji alisema tukio hilo lilitokea wakati mtuhumiwa huyo alikuwa akigombana Machi 9, mwaka huu na mzazi mwenzake, Mariam Mohamed Seleman akimtuhumu kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mwanaume mwingine.

Kamanda Mwombeji alifafanua kuwa katika tukio hilo, mtuhumiwa alimshambulia kwa kumpiga kwa fimbo ya mti wa muanzi akidai amechelewa kurudi kutoka shambani.

Alisema wakati ugomvi huo ukianza, mkewe alikuwa akitokea shambani huku akiwa amembeba mtoto wao, Amos Kassi mwenye umri wa(miezi mitatu).

Hata hivyo, alisema wakati wakiendelea na ugomvi huo, kwa bahati mbaya fimbo hiyo ilimpiga mtoto kichwani na kumsababishia maumivu makali.

Kamanda Mwombeji alisema baada ya tukio hilo, wazazi hao walimpeleka mtoto katika zahanati ya kijiji hicho kwa matibabu, lakini alifariki dunia saa 2:00 usiku siku hiyo hiyo.

Alisema mtuhumiwa huyo anatarajiwa kufikishwa mahakamni kujibu shitaka linalomkabili.

Mganga aliyeufanyia uchunguzi mwili wa marehemu, Dk. Vitalis Lusasi, alisema mtoto huyo alipata mpasuko kisogoni na kusababisha damu kuvuja ndani kwa ndani.

No comments:

Post a Comment